TAIFA TAKATIFU LAKATALIWA

TAIFA TAKATIFU LA ISRAELI LAKATALIWA

(SOMA  DANIELI  9  YOTE)

 Huu ni muendelezo wa Daniel sura ile ya nane ambapo Daniel hakupata vizuri kuielewa tafsiri yake hapa tunaendelea na hiyo tafsiri katika sura ya tisa.

Kwahiyo Gabrieli  alikuja  tena  kwa  Danieli  baada  ya  kupita  muda  fulani  tangu  siku  ile aliyozimia  ili  kumpa  maelezo  zaidi  ya  maono  yake  ya  Danieli  8.   Unakumbuka  Danieli alizimia  (Dan. 8:27).
  Kwa hiyo  Gabrieli  alishindwa  kuendelea na maelezo  yake;  sasa  akaja tena kummalizia maelezo ya maono yale (Dan. 9:20). "Muda wa majuma sabini  umeamriwa [umekatwa, umetengwa kutoka katika  kipindi kile  cha  miaka  2300]  juu  ya  watu  wako  [Wayahudi],  na  juu  ya  mji  wako  mtakatifu [Yerusalemu]....  Basi ujue na kufahamu, ya kuwa tangu kuwekwa amri  ya  kutengeneza na kuujenga upya Yerusalemu hata  zamani  zake  Masihi  aliye  Mkuu;  kutakuwa na majuma saba;  na  katika  majuma  sitini  na  mawili  utajengwa  tena  pamoja  na  njia  kuu  zake  na handaki, naam,  katika  nyakati  za taabu.    Na  baada  ya yale majuma  sitini  na mawili,  Masihi atakatiliwa  mbali....    Naye  atafanya  agano thabiti na  watu wengi  kwa  muda  wa juma  moja; na  kwa  nusu  ya  juma  hiyo  ataikomesha  sadaka  na  dhabihu..."  (Dan.  9:24-27).    Kama ilivyo, juma moja lina siku saba, na siku  moja  ya  unabii  ni  mwaka  mmoja  wa  kawaida.

 Kwa hiyo,  majuma  70  ni  siku  70  x  7  =  siku  490  au  miaka  490.    Miaka  hiyo  inakatwa katika  ile  2300  ya  Danieli  8:14  na  inaanza  kuhesabiwa  mwaka  ule  ule  wa  457  K.K. ilipotolewa  amri  iliyofanikiwa ya  kuujenga  upya  Yerusalemu.  

 Miaka  hiyo  490  kuanzia  457 K.K. inaishia mwaka 34 B.K.  Kipindi hicho walipewa Taifa Takatifu  la  Israeli  ya  kale  ili kutekeleza mambo 6 yaliyotajwa.  Walitakiwa kumpokea Masihi kama Mwokozi wao na kupewa haki yake. Lakini alipokuja kwao hawakumpokea kama Taifa (Yohana 1:11). Majuma 7 ni miaka  7  x  7  =  miaka 49  kuanzia  457 K.K.  hadi 408  K.K.  Majuma  62 ni  miaka  62  x  7  =  miaka   434  kuanzia  408  K.K.  hadi  26  1/2  au  27  B.K.    Mwaka  wa  27 ndio Yesu  akajulikana kama  Masihi  [Mpakwa Mafuta]  alipobatizwa na  kushukiwa  na  Roho Mtakatifu (Mt. 3:13-17;  Mdo. 10:38).  
Ni kweli  wakati ulikuwa "umetimia" kulingana na unabii wa  Danieli 9  uliomhusu  Masihi (Mt.  4:17).   Majuma  7  +  majuma  62  =   majuma   69 au miaka  49  +  434  =  miaka  483  tangu  457  K.K.  ambayo  iliishia 27 B.K.    Kwa  hiyo  likawa limebaki  juma  1  tu  au  siku  7  au  miaka  7  tu  kumaliza  kipindi  kile  cha  miaka  490 waliyopewa  Taifa la  Israeli kumpokea  Yesu   Miaka  490  -  483  = miaka  7  ambayo  ingeishia 34 B.K.  (27  +  7  =  34).   Katikati  ya  juma la  mwisho,  yaani,  nusu  ya miaka  7  ni  miaka  3 1/2  "Masihi atakatiliwa mbali"  atauawa kikatili.  Kwa hiyo 27 + 3 1/2 =  30  1/2  =  31  B.K. Kristo (Masihi)  alisulibiwa.   Unabii  huu ulitimia  barabara.   Ingawa  Taifa  la Israeli  lilimkataa Masihi  katakata  kuwa  sio Mfalme  wao  (Yoh.  19:15),  walikuwa wamebakiwa  na  kipindi  cha miaka 3 1/2 hadi 34 B.K. cha kuhubiriwa Injili. Siku moja  ilipokaribia   Pasaka  yake  ya  mwisho  kabla  hajaingia mjini  aliulilia  sana  mji na kuusikitikia kwa kile kitakachoupata (Mt. 19:  41-44;    Mt.  23:37-39).    Alitabiri  juu  ya kuangamizwa  kwa  mji  huo  na  majeshi  ya  Warumi  mwaka  wa  70  B.K.  (Dan.  9:26b). Walikuwa wanajivunia hekalu, lakini yeye akawaambia  wazi,  "Angalieni  nyumba  yenu mmeachiwa hali  ya ukiwa,"  yaani, utukufu  wake  umeondoka  mle  kuanzia  siku  ile.  

Hotuba yake  ndefu  ya  Mathayo  24  na  25  ilihusu  matukio  ya  siku  za  mwisho.    "Ikawa  Yesu alipomaliza maneno hayo yote, aliwaambia wanafunzi wake,  Mnajua ya  kuwa  baada  ya siku mbili  itakuwa Pasaka,  na Mwana  wa  Adamu  atasalitiwa  asulibiwe"  (Mt. 26:1,2).    Huo ulikuwa mwaka wa 31 B.K.    Kipindi  kifupi  kabla  ya  Pasaka  hiyo  alikuwa  amewaambia waziwazi kuwa "Ufalme wa  Mungu  utaondolewa  kwenu,  nao  watapewa  Taifa  lingine lenye kuzaa matunda yake" (Mt. 21:43).  Ni taifa gani hilo? Kwa nini alisema maneno hayo kwao? (Mt. 21:33-46)Taifa lingine  Takatifu  la  Israeli ni  lipi?   Lilipewa  lini Ufalme  wa Mungu?   Bila   shaka lilipewa ilipokwisha  miaka ile 490 au majuma 70 waliyopewa Taifa  la  Israeli  la  zamani. Walikuwa bado  wamebakiwa na miaka mitatu  na  nusu  ya kuhubiriwa  injili  (30 1/2  +  3  1/2 = 34).  Muasisi  wa Taifa  Jipya  la Israeli  ni Kristo  mwenyewe.   Aliwaagiza  wanafunzi  wake kuhubiri injili kwanza kwa "kondoo waliopotea wa  Israeli"  na  kuwakataza  wasiwaendee Mataifa (Mt.  10:6).  Hatimaye  aliwaambia,   "Lakini  mtapokea  nguvu,  akiisha kuwajilia  juu yenu Roho Mtakatifu;  nanyi  mtakuwa  mashahidi  wangu  katika  Yerusalemu,  na  katika Uyahudi  wote,  na  Samaria,  na  hata  mwisho  wa  nchi  [dunia]"  (Mdo.  1:8). Mwaka  34  B.K.  Stefano  alipigwa  mawe,  na  mwaka  uo  huo  injili  ikaenda  kwa Mataifa.  Mwaka uo huo Paulo akawatangazia  Wayahudi  waliomkataa  Masihi,  akasema,  "Ilikuwa  lazima  Neno la  Mungu  linenwe kwenu  kwanza  [umuhimu  wa  kwanza mpewe ninyi];  lakini kwa kuwa  mnalisukumia  mbali,  na  kujiona  nafsi  zenu  kuwa  hamkustahili uzima wa milele,  angalieni,  twawageukia  Mataifa" (Mdo. 13:46).  
Taifa  la Israeli likawa limekataliwa.   Tangu  34  B.K.  si  taifa  takatifu  tena;   wala  halijatengewa  kipindi  kingine maalum  cha  kuhubiriwa  injili  kama  upendeleo  kwao  baada  ya  kanisa  kunyakuliwa  (1 The.4:16,17[18]).  Hapatakuwa na  mwanadamu  hai duniani  kanisa  litakaponyakuliwa (Yer. 4:23-26).  Waliuchezea muda wao waliotengewa na Mungu.    Watahubiriwa  injili  pamoja na  mataifa  yote  katika  kipindi  kimoja  tu  kuanzia  34  B.K.  mpaka  Kuhani  Mkuu,  Yesu Kristo, atakapofunga kazi yake  ya  Maombezi  katika  Hekalu  la  mbinguni  (Ufu.  14:6-12;  15:8;  22:11).  Kitakachofuata ni mapigo 7 ya mwisho (Ufu. 16 yote). Masharti  yale  yale  aliyolipa Taifa Takatifu  la  Israeli la zamani ndiyo  yale  yale  aliyolipa Taifa Takatifu la Israeli ya Kiroho au Wakristo (Kut. 19:5,6;  1 Petro 2:9,10;    Ebr.  8:10).  Utii kwa Amri Kumi ndio msingi wa Agano la Kale na  Agano  Jipya.    Hii  ndiyo  maana "watakatifu" wa siku  za  mwisho  kama  wale  wa zamani  watakuwa wanazishika Amri  Kumi za Mungu pamoja na Imani ya Yesu (Ufu. 14:12;  1 Yoh. 2:3-6).  Imani ya Yesu  inahusu kumpokea kama  Mwokozi na  kufuata mafundisho yake  yote  (Mt. 28:19,20;  Mk. 16:15,16;  Yoh. 3:16;  14:21-26). Wakristo wa mataifa mbalimbali wanaitwa "Wayahudi"  au "Waisraeli" wa Kiroho (Rum.  2:28,29;   9:6-8;   Gal.  3:26-29).   Kifo  cha  Yesu  msalabani  kilifutilia  mbali  tofauti iliyokuwapo kati  ya Wayahudi na Mataifa;  wote sasa  wako sawa na wana  haki sawa kwa njia ya  kumwamini Kristo  (Efe.  2:11-22).    Tungepiga  kelele  na  kusema,  "Bwana  asifiwe!!!". Hakuna   tofauti  tena.   Chini  ya Msalaba ule wa  Kalvari  wanadamu  wote  ni  sawa.   Hakuna haja  ya  kuwatengea  kipindi  maalum  cha  kuwahubiri  injili  Wayahudi.   Wanapaswa kuhubiriwa injili  sasa;  siku ya wokovu  kwa kila mwanadamu  ni  sasa, sio  baada ya kanisa kunyakuliwa (2 Kor. 6:2).  Kulinyakua kanisa  kutaambatana  na  kuangamizwa  kwa  yule Chukizo la Uharibifu na wote wanaomwunga mkono (Dan. 9:27; Ufu. 19:11-21).hili ni hakika kwamba chukizo la uharibifu litaangamizwa na wale wote watakaounga mkono madanganyo yake ,kama haya yote umepata kuyafahamu kwa nini usijinasue katika huu uangamivu ,endelea kutafakari huu unabii ukijitoa kwa YESU pekee ndiye atakupa uzima tele katika maisha yako ,Karibu kwa sura inayofuata ,kama Ukipata swali usisite kuuliza ,Bwana akubariki.
Previous
Next Post »