VITA VIKUBWA NYUMA YA PAZIA.

VITA  VIKUBWA  VINAENDELEA   NYUMA  YA  PAZIA

(SOMA  DANIELI  10  YOTE)

Karibu tena Mpendwa katika muendelezo wa neno la Mungu tunapoendelea na sura ya kumi kwa wale wageni usijisikie umekosa masomo hapana yote yapo katika hii blog.yafungue utayapata yote ,kumbuka kuwa katika dunia hii kuna vita vikali vinavyoendelea baina ya nuru na Giza yaani Kristo na shetani ,sisi ni kama chambo katika hii vita ,kwa namna flani uchaguzi wetu katika maisha ndio unaotuweka katika upande wa Kristo au wa shetani ,usisite kufanya uchaguzi mzuri wa kumfuata Kristo unapoendelea kujifunza neno lake, Karibu na Bwana akubariki.

Rafiki kumbuka kuwa ni jambo la kutisha mno kujulishwa kwamba vita vikubwa vinaendelea nyuma  ya pazia;  havionekani kwa macho yetu ya  kibinadamu,  ingawa  matokeo  yake  tunayaona. Danieli alifunuliwa, yaani, alionyeshwa vita vikubwa hivyo visiyoonekana;  akaelewa  kile ambacho alikuwa  hajapata kukielewa siku  za  nyuma  (Dan.  10:1).    Yohana  pia  akiwa  Patmo alionyeshwa juu ya vita hivyo vikubwa kuanzia vilipoanza mbinguni  na  kuhamia  hapa duniani hadi vitakapomalizika katika vita ile ya Har-Magedoni (Ufu. 12:7-17; 16:13-16; 17:12-14;   19:11-21).  
 Kumbe  kuna  nguvu  kuu mbili  zinapambana!   -----   Mikaeli  (Kristo) na  malaika  zake,  na  Joka  (Shetani)  na  malaika  zake.   Ni  Pambano  Kuu  kweli  kweli! Wahenga walisema,  "Fahari wawili wakigombana, nyasi zinateketea."  Ndivyo ilivyo. Wanadamu ndio wanaoathirika sana  katika  Pambano  hilo.    Paulo  anasema  kwamba  sisi tumekuwa   "tamasha  kwa dunia  [malimwengu yote];   kwa  malaika na kwa  wanadamu (1 Kor. 4:9).  Tutakimbilia wapi, maskini! Ajabu ni kwamba Pambano hilo linapiganwa ndani  ya  mioyo  yetu,  japo  matokeo yake tunayaona  nje.  Tutawezaje  kujihami?   Paulo anasema  tuvae  silaha zote  za Mungu ili tupambane  na  nguvu  za giza,  si kwa  kutumia  mabavu bali  kwa  kutumia  Upanga  wa  Roho, yaani, Neno la Mungu,  na  Imani,    na  Maombi  ya  dhati  (Efe.  6:10-20).    Ayubu  hakujua kilichokuwa nyuma ya mikasa iliyompata kwa mfululizo;  lakini hatimaye alijua.   Hatujui kwa  nini  mambo  yanatuendea  vibaya  ingawa  sisi  tunaomba  sana.   Kumbe!   nyuma  ya mambo yote yanayotutatiza  kuna  vita  vikubwa  vinaendelea  kati  ya  nguvu  za  wema  na nguvu  za  uovu.   Mungu  angetufumbua  macho  yetu  wengi  wetu  tungezimia  kuona  jinsi Shetani na malaika  zake wanavyowafanya  wanadamu  au  tungekata  tamaa kabisa usishange hata katika kujifunza huu unabii jinsi changamoto ulivyoziona lakini jipe moyo Mungu atakufunulia zaidi.   Unabii wote  wa  Danieli  2,  7,  8,  9,  11,  12;    kitabu  cha  Ufunuo  chote;  Mathayo  24  unalihusu pambano  hilo  au  vita  hivyo  vikubwa.   Mungu  ashukuriwe ya  kwamba  ushindi ni  wa hakika kwa  watu  wa  Mungu hata  kama  watakatwa vichwa au kufanyiwa jeuri  yo  yote  (Ufu.  15:2; 20:4; 12:11;   Ebr. 11:35-38;  Rum.8:35-39).
Je, Shetani anafurahi watu wa Mungu wanapofanikiwa  kufanya  kazi  ya  Mungu? Hasha.  Anaweka  vipingamizi  vingi  ili  kuzuia  kazi  ya  Mungu  isifanyike  kabisa.  Kazi  ya Mungu  inamnyang'anya  raia  zake  aliodhani  ni  mateka  wake;    yeye  hataki  kuwachilia kamwe.   Kinyume na shetani ambae anataka wote wapotee.

"Asiyewafungua  wafungwa  wake  waende  kwao"  (Isa.  14:17b).    Hata  wale waliomponyoka kwenda mkononi mwa Yesu anajaribu kuwapokonya tena  (Yoh.  10:2730).  Kwa  hiyo,  ni  vita  vikubwa  vinavyoendelea  nyuma  ya  pazia  mpaka  hapo vitakapozimwa  na  Mungu  mwenyewe katika siku ile  ya mwisho.    Anaweza  kutufunulia  au anaweza  asitufunulie.   Kwetu  sasa  ni  vizuri  kuelewa  tu  kuwa  tuko  kwenye  uwanja  wa mapambano, na  kwamba "hapa  sipo  mahali  pa  raha"  yetu;   uchafu  umejaa  na  maangamizo mazito sana" (Mik. 2:10).
Tunamkuta Danieli amefunga kwa siku 21  akiomba  ili  Mungu  aifanikishe  kazi  ya ujenzi  wa  Yerusalemu kama  Koreshi alivyowatuma Wayahudi kuifanya kazi  hiyo  (Ezra 1:25).  Kazi ile  haikwenda vizuri;  kulikuwa  na  vurugu  nyingi kutoka  kwa Wasamaria  ambao hawakutaka hekalu lile lijengwe (Ezra 4).  Mashtaka yakaenda kwa Koreshi ili  atoe  amri ya  kusimamisha  kazi  ile.    Kumbe  wakati  ule  ule  alipokuwa  anaomba  Danieli,  mfalme Koreshi alikuwa anashawishiwa mawazoni mwake kuisimamisha kazi  ile.    Kumbe  vita vikubwa vilikuwa  vinaendelea  kati ya  Mikaeli (Kristo)  na  Shetani juu  ya suala hilo. 
  Kristo akimshawishi  Koreshi kuunga  mkono kazi  ile, na Shetani  akimshawishi  Koreshi  kuikataza kabisa  kazi  ile  aliyokuwa ametoa  amri.   Mapambano ya  siku  21  yakaulainisha kidogo moyo wa Koreshi.Ndipo  Mikaeli (Kristo) akaja kwa Danieli (Dan. 10:2-9;  Ufu.  1:10-15).  
 Danieli alipotelewa  na  nguvu  kabisa  mbele  za  Kristo,  akaanguka  chini  uso  ukielekea  chini  na usingizi  mzito  ukamshika.   Ndipo  Gabrieli  akamwinua  na  kumweka  katika hali ya  kusujudu na kumjulisha sababu  ya maombi yake kuchelewa  kujibiwa (Dan. 10:10).   Kumbe sala ya Danieli  ilikuwa  imesikiwa  siku  ile  ile  aliyoanza  kuomba  (Dan.  10:12).

  Kwa  nini  jibu lilicheleweshwa  basi?

  "Lakini  mkuu wa ufalme  wa Uajemi  alinipinga  siku  ishirini  na moja;  bali, tazama, huyo Mikaeli [Kristo],  mmoja wa hao  wakuu  wa  mbele,  akaja  kunisaidia; nami  nikamwacha  huko  pamoja  na  Wafalme  wa  Uajemi  [Kristo  aliendelea  kuwagusa mioyo  wafalme  wa  Uajemi  waliomfuata  Koreshi]"  (Dan.  10:13).    Gabrieli  alijaribu kumshawishi  Koreshi  kwa  siku  21  bila  mafanikio,  ndipo  akaja  Kristo  mwenyewe  na kuugusa  moyo  wa  Koreshi  ili  kazi  ya  ujenzi  wa  Yerusalemu  isikwamishwe.   Hata  sasa malaika  wa  Mungu  wanakuwamo katika Mabunge ya  nchi mbalimbali  yanayotunga sheria ili  kuhakikisha  sheria  hizo  hazitaiathiri  kazi  ya  Mungu  ulimwenguni.  
Malaika  waovu wanajaribu kuwashawishi Wabunge kutunga sheria zitakazoiathiri kazi ya Mungu;  lakini malaika wa nuru  wanapinga.  Ni  vita vikubwa  hivyo  nyuma  ya  pazia!  Ipo  haja kubwa ya kuiombea kazi ya Mungu duniani hasa, kwa wakati kama huu. Kwa nini  Kristo alikuja  kwa  Danieli wakati  kama  ule?   Kulikuwa na ujumbe kwa  ajili ya  siku  hizi  za  mwisho.    Gabrieli  akampasha  habari  Danieli,    "Sasa  nimekuja kukufahamisha mambo  yatakayowapata watu wako [Israeli ya Kiroho] katika  siku  za mwisho;    maana  maono  haya ni ya  siku nyingi  bado"  (Dan.  10:14).    Kutokana  na  maombi ya bidii ya  Danieli alionyeshwa mambo yatakayowapata watu  wa  Mungu  siku  za mwisho. Alipewa nuru ya kuyaelewa maneno ya Mungu ya kweli.    Gabrieli  alikuwa  tayari kumfunulia zaidi juu ya Maandiko, akasema,  "Lakini  nitakuambia  yaliyoandikwa  katika maandiko  ya  kweli"  (Dan.  10:21).   Neno  la  Mungu  ni  kweli;    linatutakasa  tukifanya   lisemavyo   (Yoh.  17:17;  7:17;   1  Petro  1:22-25;    Yak.  2:22).    Shetani  siku  hizi anawashawishi Wakristo wasisome Neno  la  Mungu  ati  kwa  sababu  wanaongozwa na Roho.  
Lakini  kuna  Roho  Mtakatifu  na    "roho  ya  upotevu",  nguvu  zote  mbili  zinawaongoza watu (1 Yoh. 4:1,6).  
Roho wa  kweli  kazi  yake  ni  kutufundisha  kweli,  yaani,  Neno  la  Mungu mpaka tulielewe vizuri kabisa (Yoh. 16:13-15;    14:21-26).  

Roho  ya  upotevu  inatukataza kusoma wala kusikia neno la Mungu. Yohana ametupa ruhusa  kumpima  Roho  aliye  ndani  yetu,  kujua  ni  wa  aina  gani, yaani, kama ni  Roho  wa  Mungu  kweli  au  ni  roho  ya  upotevu.  

 Mtu  anayesema  "Mimi naongozwa  na  Roho,"  halafu  anasema,  "Sina  haja  ya  kusoma,  wala  kulisikia  neno  la Mungu,"  huyo  haongozwi  na  Roho  Mtakatifu,  bali  ile  roho  ya  upotevu  au  "roho zidanganyazo," yaani, "roho  za  mashetani"  au  "mapepo"  (1  Tim.  4:1;    Ufu.  16:13,14).
 Neno la Mungu linatuimarisha sana, hata pepo zivume namna gani hazitatuangusha  (Mt. 7:24-27).   Jikite juu ya  Mwamba,  yaani,  Neno  la  Mungu  au Kristo  (Ufu.  19:13;   Yoh.1:1-3).  Neno na Kristo ni kitu  kimoja  tu.    Huwezi  kumpokea  Kristo;  na  kulikataa  Neno  lake. Usirushwe-rushwe na  kila  upepo  wa mafundisho;    omba  upewe  mafungu ya Biblia kwa  kila fundisho, utakuwa salama (Efe. 4:11-15).  Jitahidi kusoma  Biblia;    itakuhekimisha  hata upate  wokovu  wa  kweli  uliojengwa juu  ya  Neno,  sio  juu ya  hisia  na  misisimko (2 Tim.  2:15;  2 Tim. 3:15-17).

Ndugu Mpendwa hakika tuko katika Pambano NGUVU mbili zinavutana inayokuongoza kujifunza neno nyingine inakuzuia ,rafiki wewe kama wewe sio rahisi kuishinda hii vita mpaka umruhusu YESU aongoze maisha yako .Unaweza ukashuhudia upinzani uliopo unapotaka kusoma neno la Mungu ila kwa uweza wake atakuongoza utalielewa usikate tamaa .
Mungu akubariki unapoendelea kujifunza neno lake.Karibu kwa sura ya 11.
Previous
Next Post »