Karibu tena Mpendwa katika kujifunza neno la Mungu, leo kinaendelea na kitabu cha Daniel sura ya sita ambapo tutajifunza namna ambayo Mungu anavyowaongoza waendao katika kweli yake ,Karibu tujifunze .
(SOMA DANIELI 6 YOTE)
Rafiki Mpendwa tumeendelea kuufunua unabii wa Daniel katika masomo ya hapo awali tukaona kuwa Katika Babeli ya zamani na Babeli Mkuu wa mwishoe inadhihirika tabia ile ile ya Shetani ya kuichukia Sheria ya Mungu [Amri Kumi] na kuwalazimisha watu kutenda kinyume na Sheria hiyo. Waliabudu miungu, sanamu, na wafalme.
Nimrodi ndiye muasisi wa mji wa Babeli (Mwanzo 10:8-12). Aliabudiwa kama mungu Beli (jua). Beli (Isa. 46:1) ni mungu mkuu wa Wababeli na Waajemi, ni kifupi cha "Baali". Historia inaonyesha kuwa wapagani tangu siku za Babeli waliabudu jua katika siku ile ya Jumapili.
Tumeona jinsi vijana wale wanne (Danieli 1) walivyojaribiwa juu ya Amri ya Sita, isemayo, "Usiue" (Kut.20:13). Kula vyakula na kunywa vinywaji vinavyodhuru mwili ni kujiua polepole. Walishinda mtihani ule. Pia tumeona wale vijana watatu (Danieli 3) walivyojaribiwa juu ya Amri ya Pili inayokataza ibada ya sanamu (Kut. 20:4-6); walishinda mtihani ule mgumu japo walitupwa motoni.
Mungu alipendezwa kuwaokoa. Pia tuligusia juu ya kujaribiwa kwa Yusufu kule Misri juu ya Amri ya Saba, inayosema, "Usizini" (Kut. 20:14).
Alishinda. Sasa tunamkuta Danieli (Danieli 6) akijaribiwa juu ya Amri ya Nane, isemayo, "Usiibe" (Kut. 20:15). Alishinda bila shida (Dan. 6:4); alikuwa mwaminifu. Kisha tulidokeza kuwa mtihani mgumu kuliko yote wa siku za mwisho ni juu ya Amri ya Nne, inayohusu Sabato ya Mungu (Kut.20:8-11). Kizazi cha Sayansi na Teknolojia kitaweka siku ya kupumzika nyingine isiyokuwa Sabato.
Dunia itagawanyika katika makundi mawili ----- hao wazishikao Amri [Kumi] za Mungu pamoja na Imani ya Yesu, na wale wasiozishika, japo miongoni mwao watakuwamo wanaomwamini Yesu.
Kushika Amri Kumi za Mungu ni lazima uzishike zote (Kut. 20:3-17; Yak.2:10-12). "Dhambi ni uvunjaji wa Sheria [Amri Kumi]" (1 Yohana 3:4,). Tukirudi kule Babeli tunamkuta mfalme Dario aliyempenda sana Danieli, mtu wa Mungu. Kutokana na "roho bora iliyokuwa ndani yake Danieli, alimteua kuwa Waziri Mkuu wa Babeli.
Jambo hilo liliwakasirisha sana mawaziri waliokuwa wanawania cheo hicho. Wakatafuta njia ya kumwondoa katika cheo hicho kwa kuchunguza utendaji wake wa kazi na matumizi ya fedha za Dola ile ya Wamedi na Waajemi, "halikuonekana kosa wala hatia ndani yake" (Danieli 6:1-4). Wakakaa kikao cha faragha. Wakatafuta mbinu hii na ile wasiweze kuiona. Hatimaye wakasema, "Hatutapata sababu ya kumshtaki Danieli huyo, tusipoipata katika mambo ya Sheria ya Mungu wake [Amri Kumi]. Naam, wazo hilo likawa zuri na likakubalika kwa wote. Tahadhari ikawa kwamba wasiweke amri yo yote itakayomshtua mfalme maana anampenda Danieli. Wakazipitia amri moja moja wakaona ya kwanza inafaa.
Lakini Danieli hawezi kukubali kuabudu mwanadamu, maana amri hii inasema, "Usiwe na miungu mingine ila mimi" (Kut. 20:3). Wakasema mfalme atagundua tu kuwa tumemlenga Danieli, rafiki yake.
Mmoja akatoa wazo kuwa tumhusishe mfalme. Tuseme watu wote waombe kwa mfalme kwa siku thelathini tu; atajisikia vizuri, wala hatajua kuwa tumemlenga Danieli. Wakasema sisi tunajua kwamba Danieli hatakubali na tutakuwa tumemnasa kabisa, cheo cha Waziri Mkuu kitamponyoka; kitakuwa chetu. Sawa? Sawa! Wakamwendea mfalme kwa hila na kumshurutisha kuitia amri hiyo muhuri wake. Soma Danieli l6:5-9. "Basi mfalme Dario akayatia sahihi maandiko yale, na ile marufuku" (Dan. 6:9). Sheria ya Wamedi na Waajemi haiwezi kubadilika, yaani, haiwezi kubatilishwa ikiisha kutungwa mpaka itekelezwe kama ilivyo.Basi Danieli, alipojua ya kuwa yale maandiko yamekwisha kutiwa sahihi, akaingia nyumbani mwake, (na madirisha katika chumba chake yalikuwa yamefunguliwa kukabili Yerusalemu)" (Danieli 6:10). Je! aliomba kimya kimya ili watu wasisikie anaomba kwa nani? "Wakamwona Danieli akiomba dua, na kusihi mbele za Mungu wake" (Dan. 6:11).
Alikuwa anaomba kwa sauti kubwa wanasikia dua anayotoa kwa Mungu wake. Ni ujasiri ulioje mbele ya kifo kibaya cha kuliwa na simba! Yesu ameahidi kwamba "kila mtu atakayenikiri mbele ya watu, nami nitamkiri mbele za Baba yangu aliye mbinguni" (Mt. 10:32). Mkiri YESU mbele za watu naye atakukiri kwa MUNGU baba.
Danieli alipokuwa anamkiri Kristo waziwazi hata mbele ya kifo mbingu yote ilikuwa inaangalia kila kitu kwa makini sana na kujiandaa kumlinda. Wengi wetu tungekuwa tunaomba kimoyomoyo ili watu wasije wakatusikia na tukahatarisha maisha yetu. Matokeo yalikuwaje pamoja na juhudi ya mfalme kutaka amri ile isitekelezwe? "Wakamtupa katika tundu la simba" (Dan. l6:16). Wakajipongeza kuwa njama yao juu ya Danieli imefanikiwa kabisa na hawatamwona tena.
Mfalme alikuwa na imani na Mungu wa Israeli, ijapokuwa alikuwa na wasiwasi sana juu ya usalama wa maisha ya rafiki yake Danieli, alipoona wamemtupa katika tundu la simba. Akasema maneno haya, "Mungu wako unayemtumikia daima, yeye atakuponya" (Dan. 6:16). Mfalme hakulala usiku kucha akifikiria jinsi simba wanavyomrarua vipande vipande rafiki yake; akijilaumu kwa nini hakugundua njama ya mawaziri wale waliomwonea wivu Danieli. Je! simba wale wenye njaa kibao walimla Danieli, Shahidi wa Yesu? Mfalme akaenda kwenye tundu lile la simba, akilia kwa huzuni, "Ee Danieli, mtumishi wa Mungu aliye hai, je! Mungu wako, unayemtumikia daima, aweza kukuponya na simba hawa [wenye njaa]?" Danieli akamjibu mfalme, "Mungu wangu amemtuma malaika wake, naye ameyafumba makanwa ya simba nao hawakunidhuru" (Dan. 6:21,22).
Simba wale wakawa bubu; makucha yao hayakufyatuka, wala hawakuwa na ari yo yote ya kumrukia. Mfalme akaagiza wamtoe. Amri ya Wamedi na Waajemi isiyobadilika ilikuwa imetekelezwa lakini bila matokeo yaliyokusudiwa. Akatoa amri nyingine isiyobadilika ili itekelezwe mara moja. Akaamuru waliomshtaki kwa kijicho chao watupwe mle mle, "wao, na watoto wao, na wake zao" (Dan. 6:24). Nini kilitokea? "Wale simba wakawashinda wakaivunja mifupa yao vipande vipande, kabla hawajafika chini ya tundu" (Dan. 6:24). Wivu au kijicho kina mshahara wake! Wengi wanatafuta njia ya kuwang'oa wenzao kwenye vyeo vyao kwa kupeleka mashtaka ya uongo au kutega mitego ya hila ambayo huwa vigumu sana kujinasua. Mungu anaouna uovu wote huo. Wahenga walisema, "Mchimba shimo hutumbukia mwenyewe." Biblia inasema, "Mwenye kuchimba shimo atatumbukia ndani yake" (Mhu.10:8). Siku zile za Esta Hamani akamwonea wivu au kijicho Mordekai. Kwa siri akachonga mti mrefu sana wenye ncha kali wa kumtundikia Mordekai, mtu wa Mungu aliyekuwa hana hatia yo yote kama Danieli. Matokeo? Alitundikwa mwenyewe kwenye mti ule ule aliouchonga kwa mikono yake (Esta 7:
KWANZA Mfalme Dario alimpenda Mungu wa Danieli. Mungu naye akampenda mfalme huyo. Akamtuma Gabrieli kumthibitisha katika ufalme wake (Dan. 11:1). Wafalme wengi wangeiga mfano wa mfalme huyu katika kuwasaidia na kuwatetea watu wa Mungu wanaowekewa mitego ya hila ili kuwaangusha. Mungu atawabariki wafalme kama hao. Danieli akashinda mtihani ule mgumu wa kuitetea Amri ya Kwanza. Mfalme akawaandikia watu wa mataifa yote watetemeke mbele za Mungu wa Danieli. Akasema, "Yeye huponya na kuokoa, hutenda ishara na maajabu mbinguni na duniani, ndiye aliyemponya Danieli na nguvu za simba" (Dan. 6:27). Mungu anasema, "kwa maana wao wanaoniheshimu nitawaheshimu, na wao wanaonidharau watahesabiwa kuwa si kitu (1 Sam. 2:30). Danieli akafanikiwa chini ya wafalme wawili (Dan.2:28). Vijana /na watu wazima wote leo wangeiga kielelezo cha Danieli.
Leo YESU anaita kwa wale wote watakao mpokea hata waacha kamwe hata mmoja (YOHANA 6:37)anashangaa pia kwa kuna wanadamu aliowafia hawampokei mpaka anauliza leo kwako ( YOHANA 5:40) kwamba hatutaki kumfuata atupe uzima bure ,rafiki yangu toa maisha yako kwa YESU ndiye pekee aliye na uzima naye atakuongoza katika uzima tele.
Usisite kuuliza maswali ,ukihitaji kujiunga kwaajili ya kujifunza zaidi Karibu kwa kanisa la MUNGU kanisa la waadventista wa Sabato popote utakapo kuwa utajifunza zaidi MUNGU akubariki.
ConversionConversion EmoticonEmoticon