MFALME ATAKAPOHAMIA YERUSALEM

MFALME WA KASKAZINI KUHAMIA YERUSALEMU

 (SOMA  DANIELI  11  YOTE)

 Karibu Mpendwa tunapoendelea na unabii wa biblia kutoka katika kitabu cha Daniel ,kumbuka kuwa katika kila utawala au ufalme Mungu ndiye anayeruhusu hawa watawala kuongoza lakini pia Mungu hawasahau wafalme wanaofanya mapenzi yake na  kuwasaidia  watu  wake wanapopigwa vita na Shetani akitumia wanadamu kuwashtaki.   Wanadamu  wanapotaka kuivuruga au kuikomesha kazi ya Mungu, ujue nyuma yake yuko Shetani;  anawatumia.
Vita  vikubwa  [Pambano  Kuu]  vinaendelea  nyuma  ya  pazia.    Hatuwezi  kuviona  kwa macho  yetu.   Koreshi,  Mwajemi,  ndiye aliyeyaongoza majeshi  yaliyoiangusha  Babeli  usiku ule  wa  mwisho  kwa  Belshaza  (Dan.  5:25-31).   Alimwachia  utawala  wa  Babeli  mjomba wake Dario,  Mmedi.  Kama  bado  unakumbuka  masomo yaliyopita,  Dario alimpenda  sana Danieli na kumpa cheo cha Waziri Mkuu.  Pia alimpenda sana Mungu wa  Danieli.    Kwa hiyo malaika Gabrieli  alitumwa  kumthibitisha   katika kiti chake  cha enzi na  kumtia nguvu (Dan.  11:1).   Alipotawala Babeli  alikuwa mzee  wa  miaka  62;  baada  ya  kufa  kwake  Koreshi alitawala  Babeli  (Dan.  10:1).  
Katika  Danieli  11 tunaziangalia falme  zile  zile  kuanzia  Ufalme wa Wamedi na Waajemi mpaka  hapo  Ufalme wa  Kristo  utakaposimamishwa.   "Kusimama" maana  yake  kutawala.   Ufalme  wa  Babeli  ulikuwa  umeangushwa  tayari  na  Wamedi  na Waajemi. Sura  hii imeandikwa kwa  lugha  ya kawaida inayoeleweka vizuri  kwa  kila  mtu.  
 Kwa hiyo haitakuwa na shida sana katika kuuelewa ,   Unabii  huu unaendelea kutoka Sura  ile  ya  10;   Gabrieli  anazidi  kumweleza  Danieli  mambo  yatakayowapata  watu  wa Mungu  katika  siku  za  mwisho  (Dan.  10:1).   Ajabu  ni  kwamba  sehemu  kubwa  sana  ya unabii huu tayari imekwisha  timia.  Wahusika  katika pambano hili  wameelezwa wazi kwa kuonyesha vitendo vyao ambavyo vilitimia mia kwa mia.  Jukumu letu hapa ni kuwataja kwa  majina  yao  wahusika  muhimu  wachache  kutoka  katika  historia  ambao  walitimiza mafungu yaliyoonyeshwa katika mibano  mbele  ya  majina  yao.    Hebu  sasa  na  tuwapitie mmoja baada ya mwingine. Wahusika  wakuu  katika  Ufalme  wa  Wamedi  na  Waajemi:  
   Dario  (Dan.  11:1); Koreshi  (Dan.  10:1);   wafalme  watatu  wa  kwanza  waliofuatana  (Dan.  11:2)  ambao  ni Kambises, mwanawe Koreshi;   Smerdisi;  na  Dario Histaspes.    Yule  wa  nne  aliyekuwa tajiri kuliko wote ni  Ahasuero,  huyo  ndiye  aliyechokoza  vita  juu  ya  ufalme  mdogo  wa Uyunani ambao baadaye uliuangusha Ufalme wa Wamedi na Waajemi.
 Wahusika wakuu katika Ufalme  wa  Wayunani:      Iskanda  Mkuu  (Alexander  the Great)  (Dan.11:3,4)  -----   alipokufa  akingali  kijana  mbichi  hakuacha  uzao  (mtoto)  wa kumrithi.
 Kwa hiyo majenerali wake wanne  wakagawana  ufalme  wake  katika  majimbo manne (Dan.  11:4);

  majina  yao  ni  haya:
   Cassander,  Lysimachus,  Seleucus, na  Ptolemy. Katika  ukoo  wa  Seleucus  walitawala  wafalme  wengi  zaidi  ya  20  kabla  ya  Ufalme  wa Wayunani kuangushwa na Warumi.   Mmojawapo ambaye hakuwa mashuhuri kama baba yake  ni  yule  Antioko  Epifani  (Antiochus  Epiphanes  IV)  ambaye  watu  wengine wanamdhania  kuwa  ndiye  "Pembe  Ndogo"  ya  Danieli  7  na  8.    Pamoja  na  kwamba aliwatesa  Wayahudi  kwa  miaka 3  na siku  10  na  kulinajisi  Hekalu  lao,  hatimizi  vigezo  vyote vya  "Pembe Ndogo".   Alikufa vitani  mwaka  164  K.K.  ambapo  "Pembe  Ndogo" ya Danieli 8  itaondolewa  madarakani  na  Mungu  mwenyewe  (Dan.  8:25);    wala  hakupambana  na Kristo  ana  kwa  ana  kwa  vile  alikufa  kabla ya kuzaliwa Kristo,  wala  hawezi kuwa  tishio  kwa ulimwengu katika siku hizi za mwisho kama ilivyo hiyo "Pembe Ndogo" ya Danieli 7 na 8. Majenerali  hao  wanne  wa  Kiyunani  waliendelea  kupigana  wao  kwa  wao  hadi mwisho;   Seleucus  akachukua  eneo  lote  la  Mashariki  (makao  makuu  yakiwa  Siria), Kaskazini, na Magharibi  Ulaya.    Ptolemy  akaendelea  kubaki  na  eneo  la  Kusini  (Misri).Kijiografia wafalme hao wawili waliobaki wakaitwa "Mfalme wa  Kaskazini"  (Seleucus) akikaa  Siria,  na  "Mfalme  wa  Kusini"  (Ptolemy)  akikaa  Misri.  

Ukoo  wa  kila  mfalme uliendelea kutawala hadi Warumi walipoingilia kati.  Wahusika wakuu  katika  Falme  hizo mbili za Kiyunani ni hawa:   Ptolemy Philadelphus   -----  mfalme wa  kusini  (Dan.  11:6), binti yake  ni  Bernice, aliyekwenda  kuolewa  kwa    Antiochus  Theus, mfalme  wa  kaskazini aliyekuwa na mke wake wa kwanza  Laodice  (Dan. 11:6).  Laodice akijaa  wivu  alimwua kwa  sumu  Bernice,  na  mtoto  wake  mchanga  aliyemzaa,  pamoja  na  wajakazi  wake,  na mumewe.   Kaka  yake  Bernice  aliyeitwa  Ptolemy  Eurgetes,  chipukizi  la  mizizi  yake, alikwenda  kulipiza kisasi  cha  kuuawa dada  yake  kwa  mfalme  wa kaskazini  (Dan.  11:7-13). Hatimaye  Warumi  wakaingia  katika  mandhari  hiyo  ya  vita  za  kulipizana  kisasi  kwa wafalme hao wa Kiyunani. Wahusika wakuu katika Ufalme wa Warumi:
  Ufalme wa Warumi unaingia katika fungu  la  14  hadi  la  16  la  Sura  hii.   Cleopatra,  binti  wa  watu  [wa  mfalme  wa  Misri], alipelekwa  kwa  Kaisari  Julius  (Julius  Caesar)  kama  zawadi  ya  uzinzi  ili  ampendelee katika  ugomvi  wa  utawala  na  kaka  yake  (Dan.  11:17-19);    Kaisari  Augusto,  mpenda ushuru  kwa  anasa  zake  (Dan.  11:20;   Luka  2:1-6).   "Siku  zile  amri  ilitoka  kwa  Kaisari Augusto ya kwamba watu wote wa ulimwengu  watozwe  ushuru"  (Luka  2:1,  Tafsiri  ya KJV).   Yesu,  Mkuu  wa  Maagano,  aliishi  na  kuuawa  chini  ya  Kaisari  Tiberio  (Dan. 11:21,22;   Luka  3:1;   Yoh. 18:15  -  Kaisari  Tiberio).   Warumi  waliingia Palestina  na  kuwaua Wayahudi (Dan. 11:23-29).  Kusimamishwa kwa  Chukizo  la  Uharibifu  ni  mwanzo  wa Ufalme  wa  Papa  au  Upapa    (Dan. 11:31-39) katika  kipindi kile  cha  miaka  1260  cha  Zama za Giza.   Mauaji  aliyofanya kwa  watakatifu zaidi  ya milioni 50 yameelezwa katika  mafungu 32  na  33.  
 Matengenezo ya  Kanisa  (Reformation) yaliyoanzishwa mwaka 15l7  na  Martin Luther  na  kufuatiwa  na  Wana-matengenezo  wengine  yaliwapatia  maeneo  ya  kukimbilia waliokuwa wanateswa na kuuawa na Papa  (Dan.  11:34;    Ufu.  12:16;    Mt.  24:15,21,22). Kwa  njia  hiyo  mateso  na  mauaji  yali"fupizwa"  Mt.  24:22).    Katika  nchi  za  Kikatoliki yaliendelea  hadi 1798.   Ufalme wa  Kirumi wa  Kisiasa  ulioangushwa  unaendelezwa  mpaka leo chini ya  Upapa.
Mfalme wa Kaskazini wa Siku za Mwisho Kuhamia Yerusalemu:  Mfalme huyo ni tofauti na wafalme wale wa Kiyunani walioitwa "Mfalme wa Kaskazini"  na  "Mfalme  wa Kusini" kuanzia fungu la 5  hadi  la  17.    Ametajwa  katika  fungu  la  40  hadi  45.    Mambo yanayomhusu  "Mfalme  wa  Kusini"  wa  siku  za  mwisho  katika  mafungu  hayo  bado hayajabainishwa.   Dhana  zipo  nyingi.    Yesu  alisema,    "Na  sasa  nimewaambia  kabla halijatokea,  kusudi  litakapotokea  mpate  kuamini"  (Yoh. 14:29).   Unabii  unaposema  kusini ni kusini kwa mfalme huyo  wa  kaskazini;    nchi  zitakazopinduliwa  zimetajwa  pamoja  na nchi zitakazompatia  hazina.   Mfalme  wa Kaskazini  wa siku  za mwisho  ni Ufalme  wa Papa au  Upapa  utakapotawala katika  awamu  yake  ya pili  na  ya  mwisho  (Dan.  11:45;  Ufu.  17:811).  Ufalme  huo  unakwenda  kuangamizwa  vibaya  na  Mikaeli  [Kristo]  hapo atakaposimama  [atakapotawazwa  mbinguni  katika  sherehe  iitwayo  Arusi  ya  MwanaKondoo,  atakabidhiwa  Jiji  Yerusalemu  Mpya  tayari  kumkaribisha  mkewe  (kanisa) atakapomnyakua toka  duniani  wakati wa kuja  kwake mara  ya pili]  (Dan. 12:1;   Ufu. 19:6-9; 21:9,10).    Kwa hiyo,  Papa  atakapohamia Yerusalemu, "naye  ataweka hema  zake  za kifalme [makao  makuu]  kati  ya  bahari  [ya  Kati]  na  Mlima  Mtakatifu  [Mlima  wa  Mizeituni]  wa uzuri [Palestina]"  atakuwa  anautimiza unabii  huu.  Lakini  akiwa pale  "ataifikilia  ajali yake, wala  hakuna  atakayemsaidia"  (Dan.  11:45),   "naye  aenenda  kwenye  uharibifu"  (Ufu. 17:11).   Ni ajali  gani  atayopata,  ni  uharibifu  [maangamizi] gani  atapata?    Soma  Ufu.  19:11-21).ni hakika mnyama ataangamizwa kabisa na wale wote watakao ambatana naye wote wataangamizwa ,jina la Bwana litukuzwe maana hutupatia kila jambo tahadhali yake kabla halijatokea hivyo haya mambo ni hakika na kweli yanatokea wakati unaotujia ,hasa pale itakapotangazwa alama ya mnyama ndipo utengano utakapoonekana kati ya wale wanaoipokea na wale wasioipokea wito wangu kwako rafiki ni kwamba jifunze zaidi juu ya huu unabii na ule wa ufunuo, lakini usiogope maana kuna kundi kubwa la waaminio wale ambao hawatakubali kuipokea hiyo hapa ya mnyama nao hao watu watajazwa NGUVU na Mungu mwenyewe kwaajili ya kusimamia kweli yake ,kwahiyo kama ambavyo Mungu amekuwa akitembea na mashahidi wake kwa kila zama hata leo kuna watu watakaokuwa tayari kuuawa kwa kusimamia kweli ya Mungu, je wataka kuwafahamu wako hapa (ufunuo 14:12) nao watamshinda huyo joka kwa damu tu ile ya mwanakondoo ,ninapenda kukukaribisha katika kundi kubwa hili linaloipeperusha bendera ya YESU bila kupindisha ukweli ,lakini kumbuka kuwa hawa watu kwa namna flani hubezwa sana na kudharauliwa lakini ndivyo wanavyoenenda hata YESU atakapokuja watamlaki wakisema huyu ndiye tuliyemngoja kwa muda mrefu atuchukue ,Karibu katika hili kundi Mpendwa tunapoendelea katika kujifunza neno Kwa maandalizi ya utimirifu wa unabii nakisha tumngoje YESU ajapo kwa Mara ya pili.
Previous
Next Post »